IQNA

Watetezi wa Palestina

Wanasiasa wa chama cha Leba Uingereza  wataka nchi yao isitishe kuiuzia Israel silaha

23:05 - October 18, 2024
Habari ID: 3479611
IQNA – Madiwani 114 wa Muslim wa chama tawala cha Leba Uingereza wamemuandikia barua Waziri Mkuu wa Uingereza, wakitaka kuwekewa vikwazo vya mara moja vya silaha dhidi ya Israel huku vikosi vya utawala huo vikiendelea kutumia silaha na zana za viita  zinazotolewa na nchi za Magharibi kutekeleza mauaji ya kimbari huko Palestina na Lebanon.

Katika barua ya wazi, wanasiasa hawa waliochaguliwa wa chama cha Labour wanamtaka kiongozi wa chama chao, Keir Starmer, kulazimisha "kusimamishwa mara moja na kamili kwa uuzaji wa silaha kwa Israel.”
Ikiratibiwa na Mtandao wa Waislamu Katika Chama cha Leba, barua hiyo inasema, "tusiwe washiriki katika ukiukaji huu wa wazi wa sheria za kimataifa za kibinadamu."
Inaendelea hivi, "Ni wajibu wetu wa kimaadili kuchukua hatua sasa. Ndio maana tumekutana, kama Madiwani, Waislamu, na wanachama wa Leba kuitaka serikali hii ya Leba kutimiza wajibu wetu wa kimaadili kwa kusimamisha uuzaji wa silaha kwa Israel hadi wakati ambapo sheria ya kimataifa ya kibinadamu inazingatiwa na kuheshimiwa."
Mwezi uliopita, Waziri wa Mambo ya Nje wa Uingereza David Lammy alitangaza kusimamisha leseni takriban 30 za kuuza silaha kwa utawala wa Israel kati ya jumla ya takriban 350.
Orodha ya madiwani Waislamu wa chama cha Leba waliotia saini barua hiyo ni pamoja na viongozi wakuu ndani ya mamlaka za mitaa, kama vile mameya wa mitaa, naibu viongozi wa baraza, na wajumbe wa baraza la mawaziri. Waliotia saini ni pamoja na naibu kiongozi wa Baraza la Barking, Saima Ashraf; naibu kiongozi wa Baraza la Jiji la Glasgow Labour, Soryia Siddique; na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) na diwani wa Manchester, Yasmine Dar. Watia saini wengine mashuhuri ni Meya wa Rochdale, Shakil Ahmed; Meya wa Wellington, Cllr Usman Ahmed; mjumbe wa baraza la mawaziri Oldham, Shaid Mushtaq; mjumbe wa baraza la mawaziri la Wandsworth, Aydin Dikerdem; na mjumbe wa baraza la mawaziri la Birmingham kwa Mazingira na Uchukuzi, Cllr Majid Mahmood.
Haya yanajiri siku chache baada ya wabunge 21 wa chama cha Leba, wakiwemo waliosimamishwa kazi hivi karibuni, kuunga mkono hoja ya bunge inayoitaka serikali kukomesha "mauzo yote ya kijeshi kwa Israel." Kundi la wabunge, wakiongozwa na Richard Burgon, ni pamoja na Diane Abbott na mwenyekiti wa zamani wa Chama cha Leba Ian Lavery.

3490331

Habari zinazohusiana
captcha